Mtandao wa Airtel Tanzania unaomilikiwa na kampuni kubwa ya Bharti Airtel kutoka nchini India imeingia kwenye makubaliano ya kuuza minara yake yote 1,350 kwenda kampuni ya American Tower Corporation kwa bei ya mabilioni ya shillingi.
Mauzo hayo yanategemewa kukamilika kufikia mwezi wa sita mwaka huu kwa bei ya Dola milioni 179 za kimarekani (Zaidi ya Tsh bilioni 390).

Kampuni ya ATC (American Tower Corporation) inamiliki na kuendesha zaidi ya minara 97,000 duniani kote.
Je uuzwaji huu unamaanisha nini?
- Kampuni ya ATC itachukua umiliki na uendeshaji wa minara hiyo
- Airtel itaendelea kuweka mitambo yake ya mawasiliano katika minara hiyo na kuchukuliwa kama mpangaji (watalipa kodi)
- Mtandao mwingine wowote wa simu utaweza kuweka pia mitambo yake ya mawasiliano katika minara yeyote chini ya ATC. Watalipa kodi ila kwenye mkataba wa miaka 10 kati ya ATC na Airtel utahakikisha Airtel watakuwa wanalipa pango dogo ukilinganisha na wengine
Mtandao wa Airtel umekuwa unahaha katika kujiendesha kifaida tokea kuuzwa kwake na kumilikiwa na kampuni ya Bharti. Kwa takribani mwaka sasa kuna uvumi mkubwa ya kwamba kampuni ya Bharti ipo njiani kuuza biashara yake hiyo ya Afrika muda wowote kuanzia sasa.
Airtel si wa kwanza kuuza minara yao, mtandao wa Vodacom Tanzania pia walikwisha uza minara yao kwenda kampuni ya Helios Towers Africa mwaka 2013 kwa takribani dola milioni 75. Inaonekana uendeshaji wa minara ni kitu kinachoitaji nguvu nyingi kipesa na kirasilimali watu na hivyo inaonekana ni kitu kizuri kibajeti kuachia kampuni nyingine huru kuendesha biashara hiyo.
Chanzo: IPP na mitandao mbalimbali