Mwaka jana Google walitangaza kuwa wako mbioni kutengeneza mfumo wa Android ambao utafanya kazi kwa haraka na vizuri kwenye simu za kawaida (Simu zenye sifa ndogo), Mpango huu uliitwa Android Go.
Android Go ni nini?
Ni toleo spesheli la mfumo endeshi wa Android kwa simu zenye ukubwa wa RAM 1GB au chini ya hapo, yaani simu janja zenye uwezo mdogo. Toleo hili limetengenezwa kutoka toleo kubwa, ila hili halitaitaji nguvu kubwa ya simu ili kuweza kufanya kazi katika utendaji unaoridhisha.
Hii imefanywa hivi kwa kuwa Mifumo endeshi ya Android ya nyuma kwa sasa imekuwa haiendani na App nyingi na Mifumo ya Android ya sasa ni yenye kula nafasi kubwa na yenye kuhitaji simu iwe na kiasi kikubwa cha RAM hususani kuanzia RAM 2GB na kuendelea.
Kwa kuwa bado watengenezaji wa simu wanawajali wateja wenye kuhitaji simu zisizo na sifa kubwa na zenye bei nafuu ndipo Google walipokuja na wazo la kuwa na Andoid Go. Toleo la sasa limesanifiwa kutoka kwenye Android Oreo (Go Edition).
Simu itakayokuwa na Android Go itakuja na PlayStore kama kawaida na itaweza kufanya mambo yote kama ilivyo simu inayotumia mfumo wa Android ya kawaida. Pia inakuja pamoja na App za Google Maps, Google Assistant, Google Search, Gmail, na YouTube.
Ujio wa Android Go una faida kubwa sana kwa wazalishaji wa simu na kwa wateja pia. Kuwepo kwake kutaendelea kutengenezwa simu za bei rahisi sana na wale wenye vipato vya chini watamudu kununua simu janja mpya na za kisasa.
Habari njema ni kuwa Android Go itakuwa inapata maboresho kadhaa kadri inavyohitajika kufanya hivyo.
Mpango huu wa Android umewavutia kampuni ya Airtel ya india kwa kuingia ushirika na Google kwa uzalishaji wa simu za bei nafuu zenye 4G zitakazokuwa zinatumia Android Go.