Maneno haya mawili, Android na iOS yamekuwa maarufu sana katika jamii ya teknolojia, hasa kati ya watumiaji wa simu, hasa Simu Janja duniani, yakiwa ni majina ya mifumo endeshi inayotengenezwa na kampuni za Google na Apple kwa mpangilio huo.
Mfumo Endeshi ni nini hasa?
Mfumo Endeshi (Operating System) ni mfumo mama unaowekwa katika kifaa, mfano simu, tarakilishi (kompyuta) na hata vifaa vingine ili kukiwezesha kufanya kazi. Ni kupitia mfumo huu mama ndipo ambapo mifumo mingine, kama programu huweza kufanya kazi katika kifaa hicho.
Kwa sasa mfumo wa Android ndio wenye watumiaji wengi zaidi duniani kati ya hii miwili, ukiwa na watumiaji takribani Bilioni 3.8, huku wale wa iOS wakiwa kati ya 3.9B~4.5B.
Kushabiana
Mifumo hii endeshi ina ufanano katika sehemu kuu tatu nazo ni Uwepo wa Akaunti ya mtumiaji, Uwepo wa matoleo mapya katika mfumo na Uwepo wa sehemu maalumu ya kupakua programu.
- Uwepo wa Akaunti ya mtumiaji
Katika mifumo hii yote, lazima kuwepo na akaunti ya mtumiaji iliyosajiliwa katika mfumo huo ili mtumiaji aweze kutumia kifaa chenye mfumo husika. Akaunti hii huwa na taarifa za mtumiaji husika kama vile majina, anuani ya makazi, nambari ya simu, tarehe ya kuzaliwa pamoja na taarifa mbalimbali kulingana na muundo wa mfumo husika.
- Uwepo wa Masasisho mapya katika mfumo
Mifumo hii yote huwa na matoleo mapya ya mifumo hiyo kila baada ya muda fulani. Matoleo haya hulenga mabadiliko madogo madogo katika mfumo huo au mabadiliko makubwa na kamilifu katika mfumo huo kutokana na mahitaji yaliyopo kwa watumiaji na uvumbuzi unaofanyika katika makampuni hayo. Kwa sasa, Android imefikia Toleo la 17, huku iOS ikiwa toleo la 26.5.2.
- Uwepo wa sehemu maalumu ya kupakua Programu
Mifumo hii pia ina sehemu maalumu ambapo mtumiaji huweza kupakua programu mbalimbali kwa ajili ya matumizi yake. Katika Android, Sehemu hii ni Play Store, huku sehemu hiyo ikiwa App Store katika iOS. Uwezo wa kupakua programu kupitia sehemu nyingine pia upo katika mifumo hii.
No Comment! Be the first one.