Unakumbuka kipindi ambacho zaidi ya asilimia 80 ya utumiaji wa intaneti ulihusisha kutumia huduma za Yahoo? Hii ilikuwa kama haupo kwenye barua pepe ya Yahoo basi upo kwenye huduma yake ya kuchati ya Yahoo Groups na Yahoo Messenger, ila kwa sasa inaweza pita miezi na miezi bila wengi kutumia huduma za Yahoo kabisa.
Huduma ya Yahoo Messenger ilikuwa maarufu sana katika miaka ya mwishoni ya 1990 na mwanzoni wa miaka ya 2000. Yahoo Messenger ilianza kupatikana rasmi mwaka 1998.
Na sasa Yahoo wameamua kuirudisha app hiyo katika upya mkubwa huku wakijitaidi kutumia teknolojia za baadhi ya huduma walizozinunua kama vile Flickr na Tumblr katika kuboresha zaidi app hiyo.
Swali la msingi kwa sasa ni je watafanikiwa kuleta ushindani wa maana katika soko la huduma hiyo ambalo kwa sasa limejaa ushindani mkubwa sana.
App za kuchati zinazoongoza kwa sasa katika eneo la kuchati ni Facebook Messenger, WhatsApp, Skype pamoja na Viber.
- Facebook Messenger – inatakribani watumiaji milioni 600 kila mwezi
- WhatsApp – inatakribani watumiaji milioni 700 kila mwezi
Kwa sasa Yahoo Messenger itapatikana kwa simu za Android, iOS na pia kwenye mtandao kupitia Yahoo Mail.
Je ni nini kipya?
- Kujiandikisha katika huduma hiyo kutaitaji barua pepe yako ya Yahoo au namba yako ya simu – kama vile huduma zingine zilivyo basi app hiyo iyapitia simu yako au Yahoo Mail yako na kukupatia marafiki wanaotumia huduma hiyo pia
- Uwezo wa kupata na kutuma video fupi za mfumo wa GIF ndani ya app hiyo (hii inawezeshwa kupitia huduma yao ya Tumblr – ambayo inaongoza duniani kwa uwepo wa GIF nyingi zaidi)
- Pia utaweza kutuma picha za ukubwa (na ‘quality’ nzuri) bila kujali unatumia intaneti ya WiFI au ya kawaida ya mtandao wa simu. Kumbuka apps nyingine kama vile WhatsApp huwa zinapunguza quality ya picha husika kama ni kubwa.
- Utaweza kupenda ujumbe wa watu wengine kwenye mazungumzo – yaani ‘LIKE’
- Pia kama umetuma ujumbe kimakosa basi utaweza kuufuta na haijalishi kama ujumbe umeshasomwa na watu au la, utafutwa kote ulipoenda.
Wenyewe Yahoo, wanadai hawana wasiwasi wa kushindana na apps kubwa katika soko kwa sasa, wao nia yao ni kutengeneza huduma mpya ambayo watu ambao wapo tayari kujaribu kitu kilichobora zaidi watavutiwa na huduma hiyo. Hawajali kama namba ya watumiaji haitakuwa kubwa sana, ila wanachojali ni kuona maendeleo ya taratibu katika huduma hiyo.
One Comment