m-paper ni app iliyokuja juu kwa kasi sana na hii ikiwa ni pamoja na kuchukua tuzo nchini Afrika kusini, kuandikwa kwenye vyombo vya habari mbalimbali duniani kote..
App hiyo inayomsaidia mtumiaji kununua, kusoma na kutunza magazeti vyote kwa kutumia simu au tableti yake imekuwa kama ni app iliyokuja katika wakati wa muafaka kabisa. Inasemekana kuna sehemu nchini Tanzania ambapo magazeti mapya zaidi yanayowafikia huwa tayari yanakuwa ni ya siku mbili, tatu hadi nne nyuma.
Hali hii inatokana na ubovu wa miundombinu ya barabara na pia kutokana na umbali wa maeneo husika kutoka njia kuu za usambazaji.
Hili sio jambo la kipekee linaloleta umuhimu wa app ya m-Paper, kingine ni urahisi wake katika kununua na kuhifadhi magazeti kwa wale wanaopenda utunzaji wa magazeti wanayoyanunua, pia magazeti ya nakala za kidigitali yanakuwa bei rahisi zaidi. Bei inakuwa rahisi kutokana na kuondoa gharama za usambazaji na uchapishaji.
Siku chache zilizopita Mkurugenzi mkuu wa kampuni ya SmartCodes, waliotengeneza app hiyo, alitangaza rasmi ya kwamba m-Paper imekuwa rasmi sehemu ya familia ya Vodacom.
Baada ya kupata taarifa hiyo nikajua moja kwa moja kuna mabadiliko makubwa yanakuja na nikaona haitakuwa mbaya kuwasiliano na mkurugenzi huyu ili aweze kunipatia majibu ya maswali kadhaa.
Mabadiliko makubwa!
Tayari kupitia soko la apps la Google Play kuna toleo jipya kabisa la m-paper lililo na muonekano mpya. Hii ikiwa na kuichana na rangi za kijani za mwanzo na sasa imechukua rangi nyekundu – kama m-Pesa vile.
Je watumiaji wa mitandao mingine ya simu wataweza kuendelea kutumia huduma hii?
Watumiaji wa mitandao mingine wataweza kuendelea kujiandikisha kama kawaida.
Malipo je?????? Hapa ndio mabadiliko makubwa yamefanyika ambayo nadhani watumiaji wengi wa app hii ambao sio watumiaji wa mtandao wa Vodacom hawatafurahishwa nalo. Ingawa mtumiaji wa simu wa mtandao wowote ataweza kupakua app hii huduma za malipo kupitia mitandao mingine kama vile Airtel Money, Tigo Pesa n.k imeondolewa.
Huduma za malipo zitakazokuwa zinapatikana kwa sasa ni m-pesa, VISA, Mastercard na American Express. Ila mtumiaji wa m-pesa anaweza kumnunulia au kumlipia mtumiaji mwingine wa m-paper.
Je m-paper ndio imetoka kabisa kabisa kwenye mikono ya SmartCodes?
Swali langu lililenga kwenye usimamiaji na utengenezaji zaidi wa masasisho (updates) n.k, katika hili Bwana Edwin alisema ni mapema sana kuliongelea. Ila kwa mtazamo wetu tunadhani ni jambo linalofanyika kwa utaratibu na pia tusishangae ikiwa bado Vodacom wataachia SmartCodes jukumu kubwa la kuendelea kuisimamia app hiyo kimatengenezo huku wenyewe wakijikita katika kuitangaza zaidi.
Si ubishi sana ya kwamba watumiaji wa mtandao wa Vodacom ndio watakaokuwa wamenufaika zaidi na uamuzi wa Vodacom kuichukua m-paper. Ila pia faida nyingine ambayo ni kwa watumiaji wote ni urahisi wa kupata huduma ya msaada (customer care) kwa sasa ukilinganisha na zamani. Kwa sasa huduma zote kwa watumiaji wa app hiyo zitakuwa zinatolewa kupitia Vodacom.
Wengine wanaona kama vile uamuzi wa kuibana moja kwa moja app hiyo kwa uhusiano wa mtandao mmoja wa simu (kimalipo) unaweza ukawa sio uamuzi mzuri – TeknoKona tunaamini uamuzi huu unaweza ukawa umefanyika kwa kuangalia ukubwa wa kampuni ya Vodacom na nafasi kubwa iliyopo ya kutumia mabavu ya kampuni hiyo kuipaisha zaidi m-paper. Kama ni hivyo basi ni jambo jema, tujiandae kusikia m-paper ikivuka mipaka.
[Mabadiliko, mwanzo kwenye kichwa cha habari tulitumia neno ‘imeuzwa’, ni makosa….ni ‘mkataba wa kimahusiano’ (partnership) na hivyo SmartCodes wanaendelea kuwa wamiliki wa app hiyo]
No Comment! Be the first one.