Katika hali isiyotarajiwa Huawei imetangaza kuwa mfumo wake endeshi wa simu HongMeng OS si mbadala wa Android kama ilivyokuwa ikisemekana hapo awali.
Programu endesh ya HongMeng OS ilipata umaarufu sana hivi karibuni ikisemekana kuwa huenda ingetumika kama mbadala wa Android kwa kampuni hiyo. Na ingetumika kwenye simu janja zake zijazo ikiwa ni baada ya zuio la Rais wa Marekani, Donald Trump kwa makampuni ya Kimarekani kutofanya kazi na Huawei, lakini ‘ukweli’ ni kwamba mfumo huo si mbadala wa Android.
Mwenyekiti wa kampuni hiyo, Liang Hua amesema kwamba, “Mfumo huo wa HongMeng upo kwa ajili ya baadhi ya vifaa vingine lakini sio katika swala la simu janja (Smartphones)”.
Aliongeza kusema kuwa, “bado Android ni chaguo letu la kwanza na wala hatujafanya maamuzi yeyote kuhusu HongMeng kutumika kwenye simu janja hapo baadaye.”
Taarifa zinasema mfumo endeshi kwa simu za Huawei utakuwa ni mfumo endeshi jumuishi ukihusika kutumika katika vifaa mbalimbali vya kielktroniki janja (IoT).
Hata hivyo wataalamu wa mambo ya Teknolojia wanasema mabadiliko hayo ya Huawei ni ujanja wa kibiashara wa kulinda soko lake na kuendelea kujipanga zaidi kwa mfumo wake endeshi kwa siku za baadae baada ya tukio la awali la kuzuiwa kutumia Android.