Habari wadau! Tumewaeleza kwa undani kuhusu simu mbalimbali za gharama kama iPhone 6 lakini mwisho wa siku wengine hawapendi kununua simu za gharama sana, au kubwa sana. Pia hata wale wanaomiliki simu kubwa pia wanavutiwa na kumiliki simu ya pili kwa ajili namba nyingine na wanapendelea iwe ndogo. Ukiwa kwenye kundi hili, au pia kama sijagusia kundi lako naamini simu hii ya Smart Kicka kutoka Vodacom inaweza ikawa ni chaguo bora ukilinganisha sifa zake na bei ya kutupa inayouziwa.
Je hili ni dili la uhakika?
Hilo ndilo swahili muhimu ila kabla sijalijibu, tupitie vitu muhimu kuhusu simu hii.
Loading
Video ya 1 – Muonekano wa boksi | Jiunge nasi pia kupitia Instagram @teknokona
Inakuja na Android 4.4.2, hili ni miongoni mwa toleo jipya kabisa la Android, na isikutishe ukafikiria jambo hili litaifanya simu hii kutokuwa kasi, yaani kuwa ‘slow.’ Simu hii inafanya kazi kwa kasi mzuri tuu na tunategemea hii inaweza ikawa kwa sababu imetumia toleo spesheli kutoka Google linalohakikisha hakuna vitu visivyokuwa vya msingi sana kama vile ilivyokuwa kwenye simu nyingi zilizotoka mwaka huu za kisasa kama Samsung Galaxy S5 na zingenezo. Nimeichunguza na kukuta inasehemu ya kutazama kama kuna sasisho (update) jipya.
Ina uwezo wa Bluetooth na WiFI. Hii ikiwa na pamoja na kukuwezesha kutumia huduma ya ‘tethering’, ile ya kusambaza huduma ya intaneti kutoka kwenye simu ya kwako kwenda vifaa vingine. Tena mtumiaji atafurahia zaidi huduma hii kwa kuwa simu hii inashika mfumo wa intaneti ya kasi wa 3G.
Kwenye kitengo cha kamera, ina kiwango cha kawaida (2 Megapixel) na hili ni jambo la kutegemea kwa simu ya chini ya Tsh 150,000/= ila bado ni kamera ambayo ni nzuri tu kwa matumizi ya kawaida kama kujipiga viselfi na kadhalika. Tumejaribu kupiga picha eneo lenye mwanga mdogo, kupitia chaguzi la ‘Night Mode’ yaani picha za usiku kwenye kamera na iliweza kutoa picha nzuri tuu. Haina ‘flash’, yaani taa ya mwanga unapopiga picha za usiku na eneo la giza. Hivyo kwa matumizi ya picha za kawaida inaridhisha sana tuu. ila fahamu jambo moja
Kioo chake ni cha inchi 3.5, ambacho si kidogo sana kiasi cha kufanya utumiaji uwe wa shida. Maneno yanasomeka na kama unaona ni madogo bado unaweza kuongeza kupitia ‘settings’. Ni simu inayobebeka kwa uraisi na haisumbui kutumika mkononi, kwa ukubwa wa kipimo cha urefu wa mm 112 x upana mm 62 x na unene wa mm 12. Mguso (Touch) wa kioo chake unaridhisha na si wa kuzingua ukilinganishwa na ule unaokutana nao kwenye simu za bei raisi nyingi zilizopo sokoni.
Inakuja na apps mbalimbali kama Facebook, Twitter, Chrome, Gmail na nyinginezo nyingi. Utakuwa na uhuru wa kuongeza zaidi kupitia diski-uhifadhi ya simu hiyo yenye uwezo wa GB 4 na hii ni pamoja na kupewa nafasi ya kuongeza uwezo huo kupitia kadi ndogo (SD Card/Memory Card).
Ukifungua boksi linalokuja na simu hii unapata chaja, kitabu cha maelekezo zaidi (ila kwenye lugha ya Malkia Elizabeti) pamoja na ‘earphone’ zenye kiwango cha kurizisha. Kupitia utafiti wangu imetengenezwa na kampuni ya Arcatel kwa ajili ya Vodafone/Vodacom.
Simu hii inaweza kukuasaidia katika matumizi mbalimbali ya kila siku, na kutokana na kuja na Android 4.4.2 Kit Kat basi utaweza kutumia apps nyingi za kisasa. Magemu madogo mengi utaweza kuyatumia bila tatizo, tumejaribu kutumia intaneti na inafungua vizuri bila kuathiri muonekano.
Kwa sifa zote hizi tulizoangalia naweza kumalizia kwa kusema kwa bei husika, pamoja na kujumlisha 3GB za bure na dakika 1,200 hili ni dili la Uhakika. Kupitia ukurasa wao wa Facebook Vodacom wanasema simu hii unaweza ipata kwenye maduka yao. Pia kumbuka kuungana nasi kupitia Instagram – http://instagram.com/teknokona
No Comment! Be the first one.