Idadi ya watumiaji wa huduma ya intaneti inazidi kukua kwa kasi lakini bado kuna watu bilioni 4.2 kati ya idadi nzima ya watu bilioni 7.4 duniani hawana huduma ya intaneti kabisa. Namba hii ambayo ni sawa ya asilimia 43 ya watu wote duniani bado wakiwa hawapati huduma hii muhimu bado kasi ya ukuaji wa upatikanaji wa huduma hiyo ni mkubwa sana na unaotia moyo.
Pia data hizi zilizotolewa na shirika la mawasiliano la Umoja wa Mataifa (ITU – International Telecommunication Union) zimeonesha bado maendeleo makubwa yapo katika nchi zilizoendelea zaidi kiuchumi ukilinganisha na nchi maskini. Ni asilimia 35.3 tuu ya watu wanaoishi katika nchi zinazoendelea wanapata hduma ya intaneti wakati kwa nchi zilizoendelea ni asilimia 82.2. Hii ni tofauti kubwa sana! Pia katika orodha ya nchi maskini zaidi ni asilimia 9.5 tuu ya wakazi wa nchi hizo ambazo ni kama vile Zambia, ndio wanapata huduma hiyo.
Kati ya mwaka 2000 hadi 2015 watumiaji wa intaneti walikua kwa kasi kutokea asilimia 6.5 mwaka 2000 hadi asilimia 43 mwaka huu.
Kwa kiasi kikubwa ukuaji wa utumiaji wa intaneti umekua kutokana na ukuaji wa teknolojia na usambaaji wa simu za mkononi. Wakati nchi zilizoendelea nyingi zinatumia kwa kasi intaneti kupitia mfumo wa faiba (fiber) katika nchi nyingi zinazoendelea bado intaneti inategemewa kupitia mfumo wa mawasiliano ya simu hii ikiwa ni simu za mkononi na modemu.

Utumiaji wa simu katika huduma za intaneti (mobile broadband) umekua kwa mara 12 ukilinganisha na mwaka 2007, kwa sasa zaidi ya asilimia 45% ya watu duniani wanatumia huduma ya intaneti kupitia teknolojia hiyo.
Asilimia ya nyumba zenye huduma ya intaneti nyumbani imekua kutoka asilimia 18 mwaka 2005 kufikia asilimia 46 mwaka huu, 2015. Lakini kwa asilimia kubwa ukuaji huu ni kwa nchi zilizoendelea. Ila asilimia ya nyumba zenye huduma hiyo kupitia mfumo wa ‘fixed broadband’ yaani kama vile faiba (mfano mwingine ni huduma inayotolewa na makampuni kama TTCL na SimbaNet, yaani wanakuunganishia kwa waya) unakua kwa utaratibu sana, mwaka 2012 ni asilimia 7 tuu ya nyumba zilikuwa zinapata huduma ya intaneti kupitia teknolojia hii na imekua taratibu kufikia asilimia 11 tuu kwa mwaka huu.
Duniani kote maeneo ambayo huduma ya intaneti kupitia teknolojia ya 2G inaweza kupatikana imepanda tokea asilimia 58 mwaka 2001 kufikia asilimia 95 mwaka 2015.
Kufikia mwisho wa mwaka huu inategemewa kutakuwa na watumiaji bilioni 7 was simu…hii itakuwa asilimia 97 ya idadi ya watu ulimwenguni na zaidi ya yote huu utakuwa ni ukuaji mkubwa ukilinganisha na watumiaji milioni 738 wa simu waliokuwepo mwaka 2000. Na wote tunatambua ya kwamba watu wengi wanazidi kununua simu janja na hivyo wengi zaidi wataweza kupata huduma ya intaneti, hivyo ukuaji huu unaweza pia ukazidi kusaidia ukuaji wa utumiaji wa teknolojia ya intaneti.
Je ni data gani katika hizi zimekufurahisha sana? Ni nini maoni yako? Tungependa kusikia kutoka kwako, na tafadhali kumbuka kusambaza makala za TeknoKona. 🙂
No Comment! Be the first one.