Katika kile kinachoonekana kama mwanzo wa mapinduzi mapya ya kisheria kwenye ulimwengu wa kidijitali, mahakama nchini Marekani imezipata na hatia kampuni za Meta (wamiliki wa Instagram na Facebook) na Alphabet (wamiliki wa YouTube) kwa kusababisha uraibu na madhara ya afya ya akili kwa vijana.
Uamuzi huo uliotolewa na majaji mjini Los Angeles, ni mara ya kwanza kwa kampuni za teknolojia kuwajibishwa kisheria kutokana na mfumo wa utendaji (design) wa apps zao, badala ya maudhui yanayowekwa na watumiaji.
Nini Kilitokea Mahakamani?
Kesi hiyo ilifunguliwa na binti mmoja anayejulikana kama KGM, ambaye sasa ana umri wa miaka 20. KGM alidai kuwa kuanzia akiwa na umri wa miaka 6 (YouTube) na miaka 9 (Instagram), alijikuta kwenye uraibu mkubwa uliompelekea kupata msongo wa mawazo (depression), wasiwasi (anxiety), na matatizo ya picha ya mwili (body dysmorphia).
Majaji waliamua kuwa:
Meta na YouTube zilikuwa na uzembe: Kampuni hizo zilijua kuwa mifumo kama infinite scroll (kusogeza kurasa bila kikomo) na autoplay zimeundwa ili “kumkamata” mtumiaji, lakini hazikutoa onyo la kutosha.
Uzembe uliosababisha madhara: Uraibu huo ulikuwa chanzo kikubwa cha matatizo ya afya ya akili ya mlalamikaji.
Malipo ya Fidia: Majaji wameamuru kampuni hizo kulipa jumla ya Dola milioni 6 (zaidi ya Shilingi bilioni 15 za Kitanzania) kama fidia na adhabu, ambapo Meta itabeba asilimia 70 ya gharama hizo.
Kwa Nini Huu ni Uamuzi wa Kihistoria?
Kwa miaka mingi, kampuni za teknolojia zimekuwa zikijilinda kupitia sheria (Section 230) inayosema kuwa hazihusiki na kile ambacho watu wanapost. Hata hivyo, kesi hii haikushambulia “maudhui,” bali ilishambulia namna programu tumishi ilivyotengenezwa. Wanasheria walidhibiti hoja kuwa:
Infinite Scroll: Inamfanya mtumiaji asijue muda unaoenda.
Notifications: Zimeundwa kuchochea kichocheo cha Dopamine mwilini, kama vile mashine za kamari.
Algorithms: Zinazosisitiza vitu vinavyoweza kuleta madhara ili tu mtumiaji asiondoke kwenye app.
Mtazamo wa Tanzania na Dunia
Huku kukiwa na ongezeko kubwa la matumizi ya intaneti nchini Tanzania, hasa miongoni mwa watoto na vijana, uamuzi huu ni funzo kubwa. Inatoa shinikizo kwa kampuni hizi kuweka mifumo salama zaidi ya ulinzi wa watoto (Parental Controls) na kupunguza mifumo ya kilevi kwenye apps zao.
Meta na Google tayari zimesema zitakata rufaa, zikidai kuwa afya ya akili ni suala tata linalochochewa na mambo mengi ya kijamii na si app moja pekee.

No Comment! Be the first one.