Dondoo Muhimu
- Motorola ndiye aliyetengeneza simu ya kwanza ya mkononi duniani mwaka 1973.
- Nokia 3310 iliuza zaidi ya simu milioni 126 duniani.
- Motorola RAZR iliuza zaidi ya simu milioni 130 na kuwa moja ya simu zilizofanikiwa zaidi kuwahi kutengenezwa.
- Nokia iliwahi kushikilia karibu asilimia 40 ya soko la simu duniani mwishoni mwa miaka ya 1990.
- Nokia na Motorola zote mbili zilipoteza nafasi yao baada ya mapinduzi ya smartphone.
- Leo Nokia na Motorola bado zipo, lakini si tena wafalme wa soko kama zamani.
Kabla ya iPhone na Samsung Kuteka Ulimwengu, Kulikuwa na Vita vya Wafalme Wawili
Kama ulikua na simu mwanzoni mwa miaka ya 2000, kuna uwezekano mkubwa sana kwamba ilikuwa Nokia. Na kama hukuwa na Nokia, basi ulijua mtu aliyekuwa na Motorola ambayo kila mtu alikuwa akiitazama kwa wivu.
Hiki kilikuwa kipindi ambacho simu haikuwa kifaa cha kupiga picha, kuingia TikTok au kutumia ChatGPT. Simu ilikuwa simu. Kupiga simu, kutuma SMS na pengine kucheza Snake. Lakini nyuma ya zama hizo kulikuwa na vita kubwa. Vita kati ya kampuni mbili zilizokuwa zinatawala dunia ya mawasiliano. Nokia na Motorola.
Na swali ambalo bado linajadiliwa hadi leo ni moja. Nani alikuwa mfalme wa kweli?
Motorola Alianza Safari Kabla ya Wengine Wote
Watu wengi wanapofikiria historia ya simu za mkononi, wanakumbuka Nokia. Lakini ukweli ni kwamba Nokia hakuanza mchezo huu. Motorola ndiye aliyefungua mlango.
Mwaka 1973, mhandisi wa Motorola aitwaye Martin Cooper alipiga simu ya kwanza ya mkononi duniani. Wakati huo, wazo la kubeba simu mfukoni lilionekana kama filamu ya sayansi. Kwa miaka mingi Motorola alikuwa nembo ya ubunifu. Simu zake zilionekana mikononi mwa viongozi wa serikali, wafanyabiashara na watu wenye uwezo mkubwa wa kifedha.
Kuwa na Motorola wakati huo kulikuwa sawa na kubeba kifaa cha kifahari. Lakini Motorola alikuwa na changamoto moja kubwa. Alikuwa anauza teknolojia kwa wachache.
Nokia Alibadilisha Sheria Za Mchezo
Nokia aliingia na falsafa tofauti kabisa. Badala ya kuuliza jinsi ya kutengeneza simu ya kisasa zaidi, waliuliza swali rahisi zaidi:
“Tunawezaje kufanya kila mtu awe na simu?” Ndilo swali lililobadilisha historia ya mawasiliano. Kuanzia miaka ya 1990, Nokia alianza kutoa simu zilizokuwa nafuu, rahisi kutumia na zenye betri zilizodumu kwa muda mrefu.
Katika Afrika Mashariki, hilo lilikuwa jambo kubwa sana. Wakati maeneo mengi yakikabiliwa na changamoto za umeme, simu iliyoweza kukaa siku kadhaa bila kuchajiwa ilikuwa mali muhimu zaidi kuliko muonekano wake. Ndiyo maana kwa watu wengi Tanzania, Kenya na Uganda, neno “simu” lilikuwa sawa na “Nokia.”
Nokia 3310 Ikawa Hadithi Isiyokufa
Kisha ikaja Nokia 3310. Simu ambayo leo imeingia kwenye historia ya teknolojia. Nokia 3310 iliuza zaidi ya nakala milioni 126 duniani na kuwa moja ya simu zilizofanikiwa zaidi kuwahi kutengenezwa.
Lakini mafanikio yake hayakutokana na specifications. Yalitokana na uzoefu. Betri ilidumu kwa siku nyingi.
Ilikuwa rahisi kutumia. Na karibu kila mtu alikuwa amewahi kucheza Snake. Hata leo, ukiwauliza watu wengi kuhusu simu yao ya kwanza, jina la Nokia 3310 hujitokeza mara moja. Si kwa sababu ilikuwa bora zaidi kiufundi.
Bali kwa sababu ilikuwa sehemu ya maisha yao.
Motorola Alijibu Kwa Simu Ya Kuvutia Zaidi Duniani
Nokia alikuwa akitawala kwa uimara. Motorola aliamua kutawala kwa style.
Mwaka 2004 walizindua Motorola RAZR V3. Kwa viwango vya wakati huo, ilikuwa simu ya ajabu. Nyembamba. Ya kifahari. Ya kisasa. Na tofauti na kila kitu kilichokuwa sokoni.
RAZR iliuza zaidi ya simu milioni 130 duniani na kwa muda mfupi ilimrudisha Motorola kileleni mwa mazungumzo ya teknolojia.Watu wengi waliinunua kwa sababu moja.Ilikuwa inaonekana vizuri.
Katika enzi ambayo simu nyingi zilifanana, Motorola alifanya simu kuwa bidhaa ya mtindo wa maisha.
Kisha iPhone Ikafika na Kubadilisha Kila Kitu
Mwaka 2007, Apple ilizindua iPhone. Kwa nje ilionekana kama simu nyingine tu. Lakini ndani yake kulikuwa na wazo jipya kabisa. Badala ya simu kuwa kifaa cha mawasiliano, iligeuka kuwa kompyuta mfukoni.
Hapo ndipo matatizo ya Nokia na Motorola yalianza. Makampuni yote mawili yalikuwa yamezoea kushindana kwenye betri, ukubwa wa simu na ubora wa kupiga simu. Apple na baadaye Android walikuwa wanajenga dunia mpya kabisa ya apps, internet na ecosystems.
Nokia aliendelea kuamini Symbian. Motorola naye hakuwa na jibu la haraka.Ndani ya miaka michache, wafalme walikuwa wameondolewa madarakani.
Leo Wako Wapi?
Nokia bado yupo.Lakini leo anajulikana zaidi kwa miundombinu ya mawasiliano, mitandao ya 5G na teknolojia za telecom kuliko simu za watumiaji.
Motorola naye bado yupo chini ya umiliki wa kampuni ya Lenovo na anaendelea kuuza simu za Android katika masoko mbalimbali duniani. Lakini hakuna kati yao anayetawala dunia kama zamani.
Enzi hizo zimepita.
Hivyo Nani Alikuwa Mfalme Wa Kweli?
Kama tunazungumzia nani alianza mapinduzi ya simu za mkononi, jibu ni Motorola. Bila Motorola, huenda safari ya simu za mkononi isingefika ilipofika leo.
Kama tunazungumzia nani aliingia kwenye maisha ya watu wengi zaidi duniani, hasa Afrika Mashariki, jibu ni Nokia. Nokia alifanya simu kuwa kifaa cha kawaida kwa mamilioni ya watu. Motorola alibuni ndoto. Nokia aliisambaza kwa dunia. Lakini somo kubwa zaidi si kuhusu nani alishinda. Ni kwamba hata kampuni inayotawala dunia leo inaweza kuanguka kesho ikiwa haitatambua mabadiliko yanayokuja.
Na hilo linafanya swali moja kuwa muhimu zaidi leo kuliko wakati wowote:
Je, ni kampuni gani ya teknolojia ya leo inayofikiri haiwezi kushindwa, kama Nokia na Motorola walivyofikiri kabla smartphone hazijabadilisha kila kitu?
No Comment! Be the first one.