Katika hali iliyowashtua wapenzi wengi wa teknolojia, kampuni ya Samsung imetangaza rasmi kuanza kusitisha mauzo na uzalishaji wa simu yake ya Galaxy Z TriFold, ikiwa ni miezi mitatu tu tangu ilipoingia sokoni.
Simu hiyo, ambayo inajikunja mara mbili na kufunguka kuwa tableti kubwa ya inchi 10, ilionekana kama kilele cha ubunifu wa simu zinazojikunja (foldables). Hata hivyo, inaonekana safari yake imefika kikomo mapema kuliko ilivyotarajiwa.

Kwa Nini Samsung Imeamua Hivi?
Ingawa Galaxy Z TriFold ilikuwa na mahitaji makubwa na kuuzwa yote (sold out) ndani ya dakika chache kila ilipowekwa sokoni, sababu kadhaa zimepelekea uamuzi huu:
-
Gharama Kubwa za Uzalishaji: Ripoti zinasema kuwa gharama za kutengeneza kioo hicho tata na bawaba (hinges) mbili ni kubwa mno. Aidha, kupanda kwa bei ya chip za kumbukumbu (RAM na Storage) duniani kumesababisha Samsung kutopata faida yoyote kwenye simu hiyo, licha ya kuuzwa kwa bei ya juu ya $2,899 (takriban Shilingi milioni 7 hadi 8.3 za Kitanzania).
-
Simu ya “Maonesho” (Showcase): Samsung imekiri kuwa TriFold haikuwahi kulengwa kuwa simu ya watu wengi. Ilikuwa ni kifaa cha kuonyesha uwezo wa kitalamu wa kampuni hiyo dhidi ya washindani wake kama Huawei.
-
Ugumu wa teknolojia za utengenezaji: Kutokana na ufundi wake kuwa mgumu, kuzalisha simu hizi kwa wingi (mass production) imekuwa changamoto kubwa.
Je, Utaratibu wa Kusitisha Mauzo Ukoje?
Kuanzia tarehe 17 Machi 2026, Samsung imeanza kusitisha mauzo nchini Korea Kusini. Kwa soko la Marekani na mataifa mengine, mauzo yataendelea tu hadi pale mzigo uliopo ghalani utakapopotea. Tovuti rasmi ya Samsung tayari imeweka alama ya “Sold Out”, na kampuni imethibitisha kuwa hakutakuwa na mzigo mpya utakaotengenezwa.
Nini Hatima ya Simu Zinazojikunja Mara Mbili?
Licha ya TriFold kusitishwa, yote hayajapotea. Won-Joon Choi, Mkurugenzi wa operesheni wa Samsung Mobile, amedokeza kuwa baadhi ya sifa za TriFold (kama kioo kipana cha multitasking) zinaweza kuhamishiwa kwenye simu za bei nafuu zaidi za Galaxy Z Fold katika siku zijazo.
No Comment! Be the first one.