Simu zinazotumia Android zinazobeba jina la Nokia zinaweza kuja sokoni katika kipindi chochote kuanzia sasa.
Taarifa za uhakika zinaonesha kampuni ya Nokia imeingia mkataba na kampuni ya Finland ifahamikayo kwa jina la HMD Global – mkataba huo unawapa nguvu HMD Global kutengeneza simu janja zinazokuja kwa jina la Nokia.
- Kampuni ya HMD Global inaendeshwa na Bwana Arto Nummela ambaye ashawahi kuwa mkurugenzi katika kampuni ya Nokia na Microsoft.
Inasemekana kampuni hiyo tayari ina bajeti ya takribani dola milioni 500 za kimarekani kwa ajili ya kuzitangaza simu hizo (marketing budget).
Kosa lililofanywa na Nokia
Wengi waliotumia simu miaka ile ya mwanzoni mwa 2000 na kabla yake wanafahamu ni kwa jinsi gani simu za Nokia zilikuwa zimetawala soko. Kosa kubwa lililowakumba Nokia linafanana na lile lililofanywa na BlackBerry. – Kutofanya maamuzi sahihi dhidi ya USHINDANI NA UKUAJI WA SIMU ZA iPHONES NA ZA ANDROID.
Kwa kiasi kikubwa kama Nokia wangejiingiza nao katika kutengeneza simu za Android basi wangekuwa mbali sana sasa hivi, kosa lao ni kujiingiza moja kwa moja katika programu endeshaji ya Windows ambayo bado kwa wakati ule ilikuwa nyuma sana ukilinganisha na apps na mambo mbalimbali yaliyokuwa yanapatikana kwa iOS na Android.
Microsoft walinunua kitengo cha biashara cha simu na tableti kutoka ndani ya kampuni ya Nokia Corporation mwaka 2014 baada ya hapo inaonekana biashara yao kupitia simu walizozipa jina la Lumia/Windows Phone hazikufanikiwa kama walivyotegemea.
Kilichotokea
- Microsoft baada ya kununua biashara za simu za Nokia taratibu waliacha kutumia jina la Nokia na kutumia Microsoft Mobile kama sehemu ya makubaliano yao
- Kipindi chote cha mpito kampuni ya Nokia Corporation hawakutakiwa kuanzisha biashara ya simu zingine kwa kutumia jina la Nokia
- Na sasa hakimiliki ya jina hilo kwenye biashara za simu imerudi kwa Nokia Corporation
Simu za Nokia zinarudi sokoni! Tuambie je kama simu zitakuwa na uwezo mzuri na kwa bei nzuri je utajisikia furaha kununua simu ya Nokia badala ya kampuni nyingine ya simu?
[socialpoll id=”2360696″]