Wakati kampuni ya simu za mikononi ya Vodacom ikiingia katika ulingo wa intaneti yenye kasi kubwa ya 4G LTE mahasimu wao wakubwa TiGo wameendelea kutanua wigo wa huduma zao za 4G katika miji mingine mitano mikoani.
Vodacom ambayo inaongoza kwa kuwa na watumiaji wengi zaidi wa simu za mkononi wiki hii imezindua kampeni yake mpya ya #HapaKasiTu ambayo ni kampeni ya kutambulisha huduma zake za intaneti yenye kasi kubwa ya 4G.
Vodacom imezindua kampeni yake katika jiji la Dar es salaam ambako huduma hii inapatikana kwa sasa (tunategemea huduma hii itasambaa kwa haraka mikoa mingine nchini). Kwa Dar maeneo yatakayopata huduma hii ni pamoja na Kunduchi Mbezi beach Mikocheni Masaki Oysterbay Kimara Ubungo Kariakoo Mbagala na maeneo ya jirani na hayo yaliyotajwa.

Kuanza kutumia huduma hii mteja kwanza anatakiwa kuwa na simu ambayo inao uwezo wa 4G kisha mteja atatakiwa pia kuwa na laini ya simu ambayo inauwezo wa 4G na mwisho mteja ni lazima awe katika endeo ambalo huduma hii inatolewa yaani mkazi wa mbeya kwa mfano kwa sasa hataweza kupata huduma hii kwa kuwa bado haijafika huko.
TiGo kwa upande wao pia wiki hii wamezindua huduma hizi katika miji mingine mitano ambayo bado ilikuwa haijafikiwa, hatua hii inawapa changamoto kubwa Vodacom ambao bado hawajaanza kupanua wigo wa huduma za 4G LTE nchini kwani tayari wenzao wamekwisha fika katika maeneo mengi ya muhimu kibiashara na pengine wateja wengi wa Vodacom watashawishika kuuhama mtandao huu kwa kutamani intanet yenye kasi.
Miji ambayo Tigo imezindua huduma zake za intaneti yenyekasi ya 4G LTE ni Tabora, Musoma, Bukoba, Kigoma na Shinyanga, hii inaufanya kampuni hii ya simu za mkononi kuwa ndiyo yenye mtandao mkubwa zaidi wa intaneti yenye kasi ya 4G LTE Tanzania kwani wameifikia mikoa mingi zaidi. Kabla ya kufikia miji hii mitano TiGo walianza na huduma zao mwaka jana mwanzoni hapa jijini Dar kabla hawaja sambaza huduma hiyo Arusha Dodoma Mwanza Moshi na Tanga.

Kampuni ya Airtel yenyewe bado haija weka wazi ni lini hasa huduma hizi za 4G LTE zitawafikia wateja wake lakini ni wazi kwamba nao watakuwa wanapika mpango kabambe wa kuweza kuingia katika vita hii, ukiacha makampuni haya makubwa ya simu za mkononi kampuni kama vile SMART wao wamekuwa wakitoa huduma hii kwa muda mrefu katika jiji la Dar es salaam na wanayafikia maeneo mengi zaidi ya jiji hili ukilinganisha na mitandao hii mikubwa lakini pia SMART wao wanavyo vifurushi vya bei nafuu zaidi vya 4G kwa ajili ya intaneti.
Mwisho wa siku mteja ndiye atakayechagua nani yupo bora katika vita hii ya 4G LTE na ikumbukwe kufikia maeneo mengi isiwe ndio kipimo cha huduma bora ila je spidi ya intaneti unayopata kweli ni ya kasi?
Soma Pia – Fahamu Tofauti Kuu Kati ya Teknolojia za 2G, 3G, 4G n.k