Kampuni ya Airtel imefunga mitambo spesheli ya kwa ajili ya kutoa huduma ya intaneti ya ‘Wireless’ yaani WiFI katika maeneo ya Chuo Kikuu cha Dodoma, yaani UDOM.
Kulingana na taarifa zilizopo kwenye mtandao wa DailyNews, huduma hiyo iliyopewa jina la Airtel UNI WiFI itawawezesha wanafunzi na wafanyakazi wa chuoni hapo kuweza kupata huduma ya intaneti ya kasi na kwa bei nafuu zaidi.
Pamoja na huduma hiyo mtandao huo wa pili kwa ukubwa Tanzania, baada ya Vodacom umesema tayari mnara wao mpya wa pili umewashwa rasmi kwa ajili ya kuboresha upatikani wa mawasiliano kwa urahisi kwa wateja wao wa eneo la chuo hicho.
Kwa kipindi kirefu maeneo mengi ya chuo hicho ni shida sana kupata mawasiliano ya uhakika kutokana na eneo la chuo kuwa kubwa sana, pia na wingi wa watumiaji.
Watumiaji wa mitandao ya simu yeyote, wakiwa na vifaa kama vile simu, tableti au kompyuta zenye uwezo wa teknolojia ya WiFI wataweza kutumia huduma hiyo. Watakachotakiwa ni kununua bando spesheli za Uni – WiFi ambazo kwa sasa zipo za masaa 24, za wiki, mwezi na za usiku kucha.
Airtel wanategemea kuanzisha huduma kama hii katika vyuo vingine Tanzania kote.
Ushindani wa mitandao ya simu katika maeneo ya vyuo vikuu unasaidia kwa kiasi kikubwa katika kufanya gharama za mawasiliano ziwe chini kwa wana vyuo ambao wanakuwa chini ya bajeti kali sana. Karibia mitandao yote mikubwa ya simu inatoa huduma za vifurushi spesheli vya bei rahisi kwa maeneo ya vyuo.
No Comment! Be the first one.