Utakumbuka miezi kadhaa tulishawahi kuandika kuhusu kuweza kupiga simu za sauti/video kwenye WhatsApp, sasa hilo limetimima kwani kipengele cha kupiga simu kwa njia ya sauti au video kimewekwa katika makundi (WhatsApp Group).
Ingawa WhatsApp wenyewe hawajathibitisha rasmi kipengele hicho lakini tayari kinapatikana katika toleo la WhatsApp Beta. Mwezi uliopita katika mkutano wa F8 Facebook ilithibitisha ujio wa kipengele hicho mwishoni mwa mwaka huu.
Kwa kuwepo kipengele hicho kuanza kupatikana katika toleo la WhatsApp Beta ni kiashirio kwamba wakati wowote watumiaji wa WhatsApp wataanza kupata sasisho hilo.
Kawaida kipengele kipya (sasisho) chochote huanza WhatsApp Beta kama sehemu ya majaribio na kisha hufuatia watumiaji wake wa kawaida. Kwa sasa kitu hicho kinapatikana katika toleo la WhatsApp beta la 2.18.189 na v2.18.192.

Namna ya kupiga simu kwenye kundi ni kama hatua za kumpigia mtu mwingine yeyote kwenye WhatsApp, lakini hii ya kwenye kundi kutatokea kipengele cha ‘Add Participant‘ ambapo muhusika atabonyeza na atakuwa amewaunganisha washiriki wote kwenye kundi, au yule atakayepokea simu hiyo kwenye kundi pia atakuwa anaweza kuongeza washiriki wengine kwenye kundi.