Inazidi kuonekana ya kwamba uamuzi wa Facebook kuinunua app ya WhatsApp mwaka 2014 kwa dola bilioni 19 haukuwa mbaya kabisa. App ya WhatsApp yafikisha watumiaji bilioni 1.5 kwa mwezi katika kipindi cha Januari 2018.
Huu ni ukuaji wa juu sana ukilinganisha na kipindi ambacho Facebook waliinunua. Mwaka 2014 wakati Facebook wananunua app hiyo ilikuwa na wastani wa watumiaji milioni 450 kwa mwezi, na kwa siku ilikuwa ni watumiaji milioni 315.
Kwa sasa ukiacha kuwa na wastani wa watumiaji bilioni 1.5 kwa mwezi, pia kwa siku ina wastani wa watumiaji bilioni 1.
Mkurugenzi wa Facebook, Bwana Mark Zuckerberg alitoa taarifa hizo alipokuwa anatoa ripoti ya robo ya mwisho ya mwaka 2017. Katika ripoti hiyo alitoa kajembe kidogo dhidi ya app ya SnapChat.
Alisema kwa sasa app ya Instagram na WhatsApp ndio zinazoongoza kwa kipengele cha ‘Story’ kutumika, kipengele hichi cha Story kiliibwa kutoka app maarufu ya SnapChat. Bwana Zuckerberg alisema kwa sasa WhatsApp na Instagram zina zaidi ya watumiaji milioni 300 kila siku wa kipengele hicho, Snapchat ina takribani watumiaji milioni 178 tuu.